Sunday 11 May 2014

ELIMU INAWEZA KUMKOMBOA BINADAMU, HASA KAMA ATAZINGATIA IPASAVYO MASOMO YAKE. JULIUS CHARLES NI MWANAFUNZI WA DARASA LA SITA ANAYETUMIA MGUU WAKE WA KULIA KUANDIKA DARASANI KUTOKANA NA ULEMAVU ALIONAO WA MIKONO.

WANAFUNZI wa Shule ya Msingi Ikungi Mchanganyiko, kitengo cha walemavu (wasioona) wakiwa darasani kuendelea na masomo chini ya walimu wao.
MWANAFUNZI Julius Charles mlemavu wa mikono, akiwa darasani huku akiandika kwenye daftari lake kwa kutumia vidole vya mguu wake wa kulia.
Julius akitandika kitanda chake kwa kutumia mguu wake wa kulia.
Akiwa kwenye darasa la kawaida (mbele aliyeweka daftari chini huku akiandika),pamoja na wanafunzi wenzake wasiokuwa na ulemavu.
Julius akitoka darasanibaada ya kumaliza kipindi na wanafunzi wenzake wasiokuwa na ulemavu.
Mwalimu mkuu wa shule hiyo, Olvary Kamilly akiwa ofisini kwake, akizungumza na mwandishi wa habari hizi (hayupo pichani), alisema jamii ya walemavu inakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo wazazi kuwaficha majumbani, pia kuwahudumia watu wa aina hii ni gharama kubwa na akaiomba jamii kuisaidia shule hiyo kwa hali na mali.
Singida. Mei 12, 2014. KUNA methali isemayo ‘Shida huleta maarifa’ na ‘Kama hujafa hujaumbika.Julius Charles (12) ni mlemavu wa viungo, anayesoma shule ya msingi Ikungi mchanganyiko, iliyopo Wilaya Ikungi, Mkoani Singida. Ni mlemavu wa mikono, lakini kutokana na bidii darasani ameweza kumudu vyema kusoma na kuandika, hali inayomwezesha awazidi hata wenzake wazima anaosoma nao darasa la sita. Alianza elimu ya msingi mwaka 2006 kwa msaada wa mama yake aliyepata taarifa juu ya shule hiyo yenye kuchukua wanafunzi Mchanganyiko (yaani wenye afya njema) na walemavu ambao wanaishi bweni. Julius alizaliwa kijiji cha Mgungari Wilaya Bunda mkoani Mara mwaka 2002, ni mtoto wa kwanza wa bwana na bibi Charle Namwanga, lakini baba yake aliugua ugonjwa wa akili, hivyo kumtegemea zaidi mama yake, serikali na wahisani kupata mahitaji muhimu. Anamudu vyema masomo yake kutokana na ushirikiano wa walimu tangu akiwa darasa la kwanza, na sasa wenzake na walimu humsaidia kwa kukamatisha kalamu kwenye mguu wa kulia, naye huandika vyema hata kuwazidi wengine wenye mikono kamili. Licha ya kufanya vyema darasani na kushika nafasi ya tatu kati ya wanafunzi 62, Julius pia humudu kuoga na kufanya kazi nyinginezo ndogondogo, ikiwemo kutandika kitanda, lakini anatoa somo kwa walemavu kujiendeleza kimasomo ili baadaye wajikomboe kiuchumi. Kama walivyo watu wengine wenye malengo ya baadaye, ndoto ya Julius ni kuwa mwanasiasa aliyebobea, ili aweze kuwasemea walemavu wenzake akiwa bungeni. Olivary Kamilly ni mwalimu mkuu wa shule hiyo, anasema Julius ni mwanafunzi anayezingatia masomo na hushiriki madarasa yote mawili, akianza na la kawaida, kisha baadaye darasa la walemavu, ingawa pia changamoto zipo nyingi zinazoikabili shule hiyo. Mwalimu Kamilly anaiomba jamii kuacha kuwatenga watoto wenye ulemavu, badala yake wawathamini na wajitahidi kuwasomesha katika shule maalumu, ili baadaye waweze kukidhi matarajio yao. Pia ameiomba jamii kuisaidia shule hiyo ili iweze kumudu vyema kuwahudumia wanafunzi wenye matatizo ya ulemavu. Adamu Bilali ni mwalimu mlemavu wa macho na Anna Mjema ni mwalimu wa wanafunzi wenye ulemavu katika shule hiyo, wanasema kuwa jamii hiyo inakabiliwa na changamoto mbalimbali, ikiwemo ugumu wa kufundisha mlemavu kama huyu. MWISHO.

MBUNGE WA SINGIDA MASHARIKI TUNDU LISSU AKIWA AMEFUATANA NA MBUNGE WA ARUSHA MJINI GODBLESS LEMA AFANYA MKUTANO IKUNGI NA KUVALISHWA MGOLOLE NA KUPEWA MKUKI IKIWA NI ISHARA YA MTU SHUJAA.

WANANCHI wa Ikungi, Jimbo la Singida Mashariki wakimsikiliza Mbunge wa Jimbo hilo Tundu Lissu alipozungumza na Wananchi hao kwenye mkutano wa hadhara kuzungumzia mambo mbalimbali ikiwemo kuwashaishi vijana na wanawake kujiandika kwenye daftari la kudumu la kupigia kura.
TUNDU Lissu akiwa juu nya jukwaa kuwahutubia wananchi waliojitokeza kusikiliza hotuba yake aliyoitoa makao makuu ya wilaya Ikungi.
. AKILAKIWA na wananchi baada ya kuvikwa vazi la mgolole na kupewa ngao na mkuki ikiwa ni ishara ya mtu shujaa.
Singida Mei 12, 2014. MBUNGE wa Singida Mashariki Tundu Lissu amehimiza vijana, wanawake na walemavu kuzikabili changamoto zilizopo jimboni mwake kwa kujiandikisha kwa wingi kwenye daftari la kudumu la kupigia kura na kuwania nafasi balimbali za uongozi, ili watatue kero hizo wakiwa madarakani. Akizungumza na wananchi wa Ikungi Mjini, Mbunge huyo aliyeingia madarakani kupitia uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 kwa tiketi ya CHADEMA, Lissu alisema kuwa sasa umefika wakati kwa makundi hayo kuwania uongozi, badala ya kuwaachia watu wachache kujirudia kila chaguzi. “Ndugu zangu, hasa vijana na wanawake muda ukifika wa kujiandikisha hakikisheni mnatumia vizuri nafasi hii…tusione aibu kugombea nafasi hizi, tukishinda vizuri nafasi ya vitongoji, vijiji na mitaa itaturahisishia pia kushinda uchaguzi mkuu wa madiwani, wabunge na Rais hapo mwakani,”alisema Lissu. Aidha Lissu aliyechaguliwa mwishoni mwa wiki iliyopita na kiongozi wa kambi ya upinzani Freeman Mbowe kuwa waziri kivuli, wizara ya katiba na sheria (muungano), alisema wajumbe wa bunge la katiba kutoka upinzani hawatarudi kujadili muswada wa katiba, hadi hapo lugha chafu za matusi zitakapokoma bungeni. Mapema kwenye mkutano huo mbunge wa Arusha mjini Godbless Lema aliyefuatana na Lissu, aliwaeleza wananchi waliokusanyika makao makuu ya Wilaya ya Ikungi kuendelea kumpa ushirikiano mbunge wa jimbo hilo, ili aendelee kuwapigania. “Mbunge wenu ni mbunge wa taifa, mpeni nafasi afanye kazi ya kuwakomboa watanzania…akienda sehemu mbalimbali za nchi akasimama na kuzungumza, wananchi watamsikiliza na kumuelewa kwa sababu ni mtu wa watu, mpeni nafasi afanye kazi ya kuwatetea wananchi,”alisema. Katika ziara hiyo, Lissu alipokewa na wananchi wa jimbo lake katika kijiji cha Ulyampiti wilaya Ikungi akitokea bungeni Dodoma, na kuvishwa mgolole na akina mama kisha wazee wanaume wakamkabidhi ngao na mkuki, ikiwa ni ishara ya mtu shujaa. MWISHO.

Wednesday 7 May 2014

HALMASHAURI YA WILAYA MKALAMA YAPITISHA TASIMU YA SHERIA NDOGO KWA AJILI YA ADA NA USHURU KUONGEZA UFANISI WA UTEKELEZAJI WA KAZI ZAKE.

MWENYEKITI wa halmashauri Wilaya Mkalama Mkoani Singida James Mkwega akisisitiza jambo wakati wa maamuzi juu ya kupitisha rasimu ya sheria ndogo mbalimbali,ikiwemo ushuru wa kuku, samaki na mazao, wakati wa baraza la madiwani lililokutana makao makuu ya Wilaya hiyo, Nduguti.
Mwanasheria wa halmashauri ya Wilaya Mkalama Neto Mwambalasu akiwasilisha rasimu ya sheria ndogo ya ada na ushuru mbalimbali mbele ya baraza la madiwani kwenye kikao cha baraza hilo lililokutana makao makuu ya wilaya hiyo, Nduguti.
Baadhi ya madiwani wa halmashauri ya Wilaya Mkalama wakipitia makablasha yenye taarifa mbalimbali ikiwemo rasimu ya sheria ndogo kwa ajili ya ada na ushuru wa kuku, mazao na samaki ili kuiongezea halmashauri hiyo uwezo wa kutekeleza majukumu yake.
Singida Mei 07, 2014. ILI kuiongezea uwezo halmashauri ya wilaya Mkalama Mkoani Singida itaanza kutoza ushuru wa kuku,samaki na mazao mbalimbali. Mwanasheria wa halmashauri hiyo Neto Mwambalasu aliwaeleza wajumbe wa mkutano wa baraza la madiwani lililokutana Nduguti kuwa, utekelezaji wa ushuru huo utaanza kutozwa baada ya kusainiwa na waziri mwenye dhamana, waziri mkuu Mizengo Pinda. Hata hivyo baadhi ya madiwani walionyesha wasiwasi kuhusiana na ushuru wa kuku, lakini mwansheria huyo aliwatoa mashaka kwa maelezo kuwa, sana sheria hiyo itawahusu wafanyabiashara wanaonunua na kusafirisha au kuvusha nje ya Wilaya hiyo. “Nawaomba sana waheshimiwa msipate wasiwasi kuhusiana na rasimu hii…mfano!, ushuru wa kuku wa Sh.500 kwa kuku, hautamhusu moja kwa moja mwananchi wa kawaida, badala yake utahusisha zaidi wafanyabishara wanaonunua na kusafirisha kuku wengi, kwa ajili ya biashara,”alifafanua. Mazao mengine yanayoingia kwenye rasimu na kiwango kikiwa katika mabano ni, samaki aina ya perege (Sh. 300), kambale (Sh. 50), kamongo (Sh.50), ng’ombe, nguruwe na punda (Sh. 2,000), wakati mbuzi na kondooo watalazimika kulipiwa ushuru wa Sh.1,000, kwa mmoja. Kwa mujibu wa Mwansheria huyo, baadhi ya ada na ushuru huo mwingine utakaohusisha maeneo 18, ni mazao ya chakula na biashara, vizimba sokoni, machinjio, ushuru wa madini, ada ya idhini ya ujenzi, mazao ya nyuki na ushuru wa kupaki/kuegesha magari. Katika hatua nyingine, baraza hilo lilipitisha mapendekezo ya kuyagawanya baadhi ya maeneo kwa kuyapandisha hadhi, ikiwemo vitongoji, vijiji, kata na tarafa, ili kutoa fursa kwa wananchi kunufaika na huduma bora baada ya kusogezwa karibu zaidi. Baadhi ya maeneo yaliyopendekezwa kuwa kata ni Mkalama, Nkalakala, Kidarafa, Tatazi, Lukomo, Tumuli, Lyelembo, Ikungu, Kinampundu, Nkungi, Dominiki na Endasiku, wakati tarafa zitakazoongezeka ni Mwanga, Gumanga na Mkalama (iliyobadilishwa kutoka Ibaga kuwa Mkalama). MWISHO.

Monday 5 May 2014

KLABU YA WAANDISHI WA HABARI MKOA WA SINGIDA-SINGPRESS IMEKABIDHI MSAADA WA KIBINADAMU KWA SHULE MAALUMU YA IKUNGI MCHANGANYIKO YENYE WALEMAVU WA AINA MBALIMBALI WAPATAO 104

MWALIMU mkuu wa shule ya msingi Ikungi Mchanganyiko iliyopo wilaya Ikungi Mkoani Singida, Bw. Olvary Kamilly (kulia) akipokea sehemu ya msaada kutoka kwa mwenyekiti wa klabu ya waandishi wa habari mkoa Singida ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya uhuru wa vyombo vya habari duniani, wakati klabu hiyo ilipoamua kuadhimisha kwa kusaidia shule hiyo yenye wanafunzi 1,200, kati yao 104 wenye ulemavu aina mbalimbali. Msaada huo umejumuisha vitu mbalimbali ikiwemo sukari, unga wa sembe, ngano, kalamu, madaftari, ndoo za maji, mafuta ya kula, biskuti, pipi, sabuni za kufulia, sahani, vikombe nk, katika makabidhiano yaliyofanyika shuleni hapo.
Elisante John, Singida Mei, 2014. WALEMAVU wamekuwa wakinyanyaswa, kubaguliwa hata kutengwa kutokana na mwonekano wao tu tangu kuzaliwa, lakini katika kukabiliana na tatizo hili serikali imekuwa ikiwapatia elimu kuanzia shule ya awali hadi elimu ya juu, lengo ni kuiwezesha jamii hiyo kupata fursa zaidi ya ajira ndani na nje ya nchi. Shule ya msingi Ikungi mchangayiko iliyopo Wilaya Ikungi Mkoani Singida ni kati ya shule hizo chache za bweni nchini inayotoa taaluma kwa walemavu mbalimbali, wakiwemo wasioona, albino na viungo. Mwalimu mkuu wa shule hiyo Olvary Kamilly anawaeleza wanahabari wa Mkoa Singida waliofika shuleni hapo kukabidhi msaada wa kibinadamu uliogharimu zaidi ya Sh.laki nane, kama sehemu ya maadhimisho ya siku ya uhuru wa vyombo vya habari duniani kuwa kitengo hicho kilianzishwa mwaka 1980. Kamilly anasema kuwa shule hiyo pia inajumuisha wanafunzi wasiyo walemavu, ambao jumla yao kwa pamoja wanafikia wanafunzi 1,200, wakiwemo wavulana 458 na wasichana 646, huku walemavu pekee idadi yao ni 104. Alisema kati ya wanafunzi hao, Jumanne Ramadhani ni mlemavu wa macho na Julius Charles mlemavu wa mikono (hana kabisa mikononi), lakini ameonyesha uhodari mkubwa wa kuandika kwa kutumia miguu yake, huku Jumanne akisoma kwa ufasaha kwa kupapasa maandishi. Kwa upande wake Mwenyekiti wa klabu ya waandishi wa habari mkoani Singida Seif Takaza alipongeza jitihada zinazofanywa na walimu na wanafunzi wa shule hiyo katika kuhakikisha jamii ya walemavu inaandaliwa kwa ajili ya kukabili maisha ya kujitegemea siku za usoni. Takaza alisema kuwa msaada huo kutoka kwa wanahabari wa mkoa wa Singida ni mwendelezo wa klabu hiyo kusaidia watu wa makundi mbalimbali maalumu yanayoodhani kuwa yametengwa na jamii. Naye Juma Issah ambaye ni mwanafunzi mlemavu wa ngozi, kwa niaba ya wenzake wote aliwashukuru wanahabari wa mkoa wa Singida kutokana na ukarimu waliouonyesha mpaka wakachukua uamuzi wa kushirikiana nao katika maadhimisho hayo. Msaada huo, unga wa sembe, ngano, sabuni, mchele, madaftari, kalamu, mafuta ya kula, pipi, biskuti, sahani, vikombe,ndoo nk, ikiwa ni mwendelezo wa wanahabari hao kusaidia makundi maalumu, kama walivyofanya hivyo mwaka juzi kwa kusaidia jamii ya Wahdzabe, inayoishi wilaya ya Mkalama. MWISHO.

Thursday 1 May 2014

RAIS MSTAAFU AWAMU YA TATU BENJAMEN MKAPA, KUPITIA MFUKO WAKE WA TAASISI YA BENJAMIN MKAPA HIV.AIDS AMEKABIDHI NYUMBA 30 ZA WATAALAMU WA AFYA VIJIJINI MKOANI SINGIDA ZILIZOGHARIMU SH. 1,945,187,143

RAIS wa awamu ya tatu Benjamen Mkapa (katikati) mkuu mkoa Singida Dk. Parseko Kone (kushoto) na mwakilishi wizara ya afya na ustawi wa jamii Dk. Catherine Joachim, akizindua nyumba ya watumishi wa afya vijijini, kati ya 30 zilizogharimu zaidi ya Sh. Bilioni 1.9 kupitia mfuko wa ‘Mkapa Foundation’ kwa wilaya za Mkalama, Iramba, Singida, Ikungi na Manyoni Mkoani Singida.
Mkuu Mkoa Singida Dk. Parseko Kone akikabidhi hati ya nyumba kwa mganga mkuu Wilaya Iramba Dk.Japhet Simeo, baada ya rais mstaafu Benjamen Mkapa kukabidhi nyumba 30 za kisasa kwa ajili ya watumishi wa afya vijijini, zilizojengwa na taasisi ya Mkapa foundation, kwa wilaya za Mkalama, Iramba, Manyoni, Ikungi na Singida, kwenye makabidhiano yaliyofanyika kijiji cha Senenemfuru katika halmashauri ya wilaya Singida.
Rais awamu ya tatu, Benjamen Mkapa akikabidhiwa kibuyu na akina mama wa kijiji cha Senenemfuru Singida vijijini, kikiwa na maana ya upendo, kwenye hafla ya kukabidhi nyumba, kati ya 30 zilizojengwa na Mkapa foundation kwa halmashauri tano za mkoa wa Singida.
Mwonekano wa nyumba iliyojengwa na taasisi ya Benjamen Mkapa katika kijiji cha Senenemfuru halmashauri ya wilaya Singida, kati ya 30 zilizojengwa katika wilaya tano mkoani Singida kwa ajili ya watumishi wa afya vijijini kwa gharama ya Sh.1,945,187,143.
Na Elisante John, Singida April 01, 2014. RAIS mstaafu awamu ya tatu Benjamen W. Mkapa kupitia taasisi yake ‘Benjamen William Mkapa HIV/AIDS’ (BMAF), amekabidhi nyumba 30 zilizojengwa kwenye zahanati 13 na vituo vya afya viwili kwa gharama ya zaidi ya Sh. Bilioni 1. 9, katika halmashauri tano za Wilaya Mkoani Singida. Akikabidhi sehemu ya nyumba hizo kwenye hafla iliyofanyika kijiji cha Senenemfuru Singida vijijini, mzee Mkapa alishukuru wafadhili waliowezesha kazi hiyo, ukiwemo mfuko wa dunia wa kupambana na Ukimwi, kifua kikuu na malaria (Global fund), kwa kuonyesha imani na serikali ya Tanzania. “Binafsi ninafarijika kufahamu kwamba wananchi wanaohudumiwa na zahanati 15 ambazo nyumba hizi zimejengwa, wataendelea kufaidika na huduma bora za afya kutoka vituo hivyo kwa sababu watoa huduma wameboreshewa mazingira ya kazi zao,”alisema rais mstaafu. Nyumba hizo zimejengwa katika zahanati ya Misughaa na Mangonyi (Ikungi), Mkenge, Mpambaa na Senenemfuru (Singida), Ulemo Uwanza na kituo cha afya Ndago (Iramba), Kinyambuli na Dominiki (Mkalama), pia kituo cha afya Itigi, Idodyandole, Heka, Mpola na Chibumagwa (Manyoni). Baada ya kukabidhi, mzee Mkapa alitumia fursa hiyo kuhimiza halmashauri za wilaya husika kutunza vyema nyumba hizo na kutumika kwa matumizi yaliyokusudiwa na alizitaka kutenga bajeti ya kutosha kwa ajili ya matengenezo ya mara kwa mara ili zidumu, kuendelea kuwa madhubuti na kuvutia zaidi. “Hata hivyo, ili kuweza kuwa na huduma ya afya bora zaidi na kamilifu ni lazima kuwepo na zahanati yenye dawa, vifaa vya kutolea huduma na vipimo na uwepo wa wataalamu wa kutosha kulingana na ikama…wekeni mkakati kuhakikisha hayo yote yanazingatiwa na kutekelezwa,”alisisitza Mkapa. Kwa upande wake mwakilishi wizara ya afya na ustawi wa jamii Dk. Catherine Joachim aliishukuru taasisi hiyo na akasema kupitia mradi huo kwa mwaka wa pili sasa utahusisha ujenzi wa nyumba 220 za watumishi wa afya kwa mikoa ya Arusha, Ruvuma, Manyara, Pwani na Singida. Aliishukuru taasisi ya Mkapa kutekeleza kazi zake kwa ushirikiano mkubwa na serikali, mashirika binafsi, wadu wa maendeleo na jamii kwa ujumla, ikiwa na lengo la kuimarisha huduma za Ukimwi, afya ya mama na mtoto na masuala mengine ya afya kwa wataalamu waliopo maeneo ya vijijini. Aidha, afisa mtendaji mkuu wa taasisi Benjamen Mkapa Dk. Ellen Mkondya-Senkoro alisema kuwa BMAF mkoani Singida imekuwa ikichangia shughuli mbalimbali ikiwemo kuimarisha huduma za Ukimwi, afya ya uzazi na masuala ya watumishi wa afya tangu mwaka 2006. Aliyataja mafanikio mengine mkoani hapa kuwa ni pamoja na kuajiri watumishi wa afya 28, kufadhili wanafunzi tisa wanaosoma vyuo mbalimbali vya afya, kujenga wodi ya wazazi katika vituo vya afya, kusaidia magari matatu ya kubebea wagonjwa na kutoa mafunzo juu ya usimamizi wa raslmali watu. MWISHO.