Sunday 7 December 2014

BENKI YA NMB, TAWI LA SINGIDA IMESHEREHEKEA SIKU YA KUJUMUIKA NA WAFANYAKAZI WOTE, 'NMB FAMILY DAY', KWA AMANI, NA KUFANA KWA KIWANGO KIKUBWA, HUKU WAFANYAKAZI WAKE WAKILA, KUNYWA NA KUFURAHIA KUPITIA MICHEZO MBALIMBALI

SHEREHE KWA WAFANYAKAZI WA BENKI YA NMB, TAWI LA SINGIDA JINSI ZILIVYOFANA KATIKA VIWANJA VYA HOTELI YA KBH, ILIYOPO ZIWA SINGIDANI.
BENKI ya NMB, Tawi la Singida imefanya sherehe kubwa kwa ajili ya siku ya wafanyakazi wake, ‘NMB Family’, iliyofanyika katika hotel ya KBH mjini Singida na kufana kwa kiwango kikubwa. Licha ya familia hizo kukutana pamoja, pia yalifanyika mashindano mbalimbali, ikiwemo kufukuza kuku (wanaume na wanawake), mpira wa miguu (wanaume) na muziki (dansi) kwa watoto. Hata hivyo watoto wawili wa mtumishi wa benki hiyo, Bw. Joseph, walifanikiwa kushinda baada ya kusakata vyema muziki wa kizazi kipya na kupewa zawadi mbalimbali na meneja wa tawi hilo, Bibi.Christine Mwangomo. MWISHO

BENKI YA NMB, TAWI LA SINGIDA IMEKABIDHI WATEJA WAKE WAWILI ZAWADI YA BAISKELI, BAADA YA KUSHINDA SHINDANO LILILOANZISHWA NA BENKI HIYO KWA AJILI YA WATEJA WANAOWEKA FEDHA KUPITIA AKAUNTI ZAO, KWENYE BENKI HIYO

MENEJA wa benki ya NMB, Tawi la Singida Bibi. Christine Mwangomo (kulia, akimpa mkono wa hongera mmoja wa wateja kati ya wawili, walioshinda shindano na weka ushinde (mwingine aliyeshinda ni mwanamke lakini hayupo kwenye picha), baada ya kuweka fedha kwenye akaunti yake na kujishindia baiskeli mpya. katikati ni meneja msaidizi wa tawi hilo, Bw. Makoyi.

MBUNGE VITI MAALUMU (CCM) MKOA WA SINGIDA, MARTHA MLATA AMEISAIDIA SEKONDARI YA NDUGUTI SH.MILIONI TATU KUONDOA TATIZO LA MAJI SHULENI HAPO

MBUNGE viti maalumu (CCM) Mkoa wa Singida, Martha Mlata ametoa msaada wa shilingi milioni tatu kwa sekondari ya kata ya Nduguti, wilaya ya Mkalama mkoani Singida, kwa ajili kuodoa tatizo la maji linaloikabili shule hiyo kwa muda mrefu sasa. Alilazimika kutoa kiasi hicho, baada ya kusomwa risala kwenye mahafali ya sita ya shule hiyo, kwamba inakabiliwa na changamoto nyingi, mojawapo ikiwa ni tatizo la maji, ambalo husababisha wanafunzi kupoteza muda mwingi kusaka maji, badala ya kushiriki masomo. Hata hivyo Mlata aliitaka halmashauri ya wilaya ya Mkalama kuhakikisha nayo inachangia kiasi cha fedha kitakachopungua, ili kazi ya kuvuta maji kwa kutumia mtandao wa bomba iweze kukamilika haraka, na yeye akabidhiwe mapema januari mwakani wakati shule zitakapofunguliwa. Licha ya kutoa kiasi hicho cha fedha, Mlata alikabidhi pia mipira na jezi za mchezo wa soka, kwa ajili ya wasichana na wavulana wa shule hiyo, msaada uliogharimu zaidi ya Sh.laki mbili na nusu. MWISHO.

SERIKALI YA MKOA WA SINGIDA IMETAKIWA KUMALIZA HARAKA MIGOGORO YA MIPAKA ILI KUWEZESHA UCHAGUZI WA SERIKALI ZA MITAA HAPO DISEMBA 14, 2014, KUFANYIKA KWA AMANI

Na Elisante John, Singida SERIKALI imetakiwa kutatua migogoro ya mipaka, ili kufanikisha zoezi la uchaguzi wa serikali za mitaa, utakaofanyika disemba 14, 2014. Rai hiyo imetolewa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Singida, kupitia mwenyekiti Mgana Msindai na katibu wake Mary Chatanda, wakati wa kikao cha kamati ya ushauri cha Mkoa. “Mheshimiwa mwenyekiti, iwapo tatizo hili litaondolewa, nina uhakika wananchi wetu watashiriki vyema zoezi la uchaguzi wa serikali ya mitaa, utakaofanyika hivi karibuni,”alisema Chatanda. Msindai alibainisha kuwa, tatizo hilo limekithiri mkoani Singida, kuanzia ngazi ya kitongoji, vijiji, kata, wilaya, pia kati ya mkoa wa Singida na baadhi ya majirani zake, ikiwemo wilaya ya Uyui, mkoani Tabora. Aliiomba serikali kumaliza haraka tatizo hili, ili wananchi waweze kushiriki vyema uchaguzi wa serikali za mitaa, ambao baadhi ya wananchi wapo hatarini kupiga kura, kutokana na kukithiri kwa migogoro hiyo. Aidha mbunge viti maalumu (CCM) Mkoa Singida, Mathar Mlata aliomba fedha za upimaji ardhi zinapopatikana kwa kila halmashauri, zikafanye kazi katika maeneo ya vijiji, badala ya kuanza na makao makuu ya wilaya. Makamu mwenyekiti halmashauri wilaya Singida, Elia Digha aliitaka serikali kutatua mgogoro wa mpaka, kati ya manispaa Singida na wilaya yake, katika eneo la Njiapanda, ambako kuna mnada maarufu, kila siku ya jumamosi. Akijibu hoja hiyo, katibu tawala mkoa Singida, Liana Hassan alisema serikali inatambua tatizo hilo, akawaomba wajumbe kuvumilia wakati huu, ambao jitihada zinafanyika, ili kutatua kero hiyo. “Tatizo hili limekuwa likishughulikiwa kwa muda sasa…nawaomba sana wajumbe muendelee kuwa wavumilivu, baada ya uchaguzi utatuzi wa migogoro hii itakuwa imepatiwa ufumbuzi,”alisema. Akihitimisha, mkkuu wa mkoa wa Singida, Dk. Parseko Kone aliagiza wakuu wa wilaya na sekretarieti ya mkoa kumaliza tatizo hilo haraka, pia mgogoro wa mpaka kati ya wilaya za Manyoni (Singida) na Sikonge (Tabora). MWISHO.

Sunday 11 May 2014

ELIMU INAWEZA KUMKOMBOA BINADAMU, HASA KAMA ATAZINGATIA IPASAVYO MASOMO YAKE. JULIUS CHARLES NI MWANAFUNZI WA DARASA LA SITA ANAYETUMIA MGUU WAKE WA KULIA KUANDIKA DARASANI KUTOKANA NA ULEMAVU ALIONAO WA MIKONO.

WANAFUNZI wa Shule ya Msingi Ikungi Mchanganyiko, kitengo cha walemavu (wasioona) wakiwa darasani kuendelea na masomo chini ya walimu wao.
MWANAFUNZI Julius Charles mlemavu wa mikono, akiwa darasani huku akiandika kwenye daftari lake kwa kutumia vidole vya mguu wake wa kulia.
Julius akitandika kitanda chake kwa kutumia mguu wake wa kulia.
Akiwa kwenye darasa la kawaida (mbele aliyeweka daftari chini huku akiandika),pamoja na wanafunzi wenzake wasiokuwa na ulemavu.
Julius akitoka darasanibaada ya kumaliza kipindi na wanafunzi wenzake wasiokuwa na ulemavu.
Mwalimu mkuu wa shule hiyo, Olvary Kamilly akiwa ofisini kwake, akizungumza na mwandishi wa habari hizi (hayupo pichani), alisema jamii ya walemavu inakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo wazazi kuwaficha majumbani, pia kuwahudumia watu wa aina hii ni gharama kubwa na akaiomba jamii kuisaidia shule hiyo kwa hali na mali.
Singida. Mei 12, 2014. KUNA methali isemayo ‘Shida huleta maarifa’ na ‘Kama hujafa hujaumbika.Julius Charles (12) ni mlemavu wa viungo, anayesoma shule ya msingi Ikungi mchanganyiko, iliyopo Wilaya Ikungi, Mkoani Singida. Ni mlemavu wa mikono, lakini kutokana na bidii darasani ameweza kumudu vyema kusoma na kuandika, hali inayomwezesha awazidi hata wenzake wazima anaosoma nao darasa la sita. Alianza elimu ya msingi mwaka 2006 kwa msaada wa mama yake aliyepata taarifa juu ya shule hiyo yenye kuchukua wanafunzi Mchanganyiko (yaani wenye afya njema) na walemavu ambao wanaishi bweni. Julius alizaliwa kijiji cha Mgungari Wilaya Bunda mkoani Mara mwaka 2002, ni mtoto wa kwanza wa bwana na bibi Charle Namwanga, lakini baba yake aliugua ugonjwa wa akili, hivyo kumtegemea zaidi mama yake, serikali na wahisani kupata mahitaji muhimu. Anamudu vyema masomo yake kutokana na ushirikiano wa walimu tangu akiwa darasa la kwanza, na sasa wenzake na walimu humsaidia kwa kukamatisha kalamu kwenye mguu wa kulia, naye huandika vyema hata kuwazidi wengine wenye mikono kamili. Licha ya kufanya vyema darasani na kushika nafasi ya tatu kati ya wanafunzi 62, Julius pia humudu kuoga na kufanya kazi nyinginezo ndogondogo, ikiwemo kutandika kitanda, lakini anatoa somo kwa walemavu kujiendeleza kimasomo ili baadaye wajikomboe kiuchumi. Kama walivyo watu wengine wenye malengo ya baadaye, ndoto ya Julius ni kuwa mwanasiasa aliyebobea, ili aweze kuwasemea walemavu wenzake akiwa bungeni. Olivary Kamilly ni mwalimu mkuu wa shule hiyo, anasema Julius ni mwanafunzi anayezingatia masomo na hushiriki madarasa yote mawili, akianza na la kawaida, kisha baadaye darasa la walemavu, ingawa pia changamoto zipo nyingi zinazoikabili shule hiyo. Mwalimu Kamilly anaiomba jamii kuacha kuwatenga watoto wenye ulemavu, badala yake wawathamini na wajitahidi kuwasomesha katika shule maalumu, ili baadaye waweze kukidhi matarajio yao. Pia ameiomba jamii kuisaidia shule hiyo ili iweze kumudu vyema kuwahudumia wanafunzi wenye matatizo ya ulemavu. Adamu Bilali ni mwalimu mlemavu wa macho na Anna Mjema ni mwalimu wa wanafunzi wenye ulemavu katika shule hiyo, wanasema kuwa jamii hiyo inakabiliwa na changamoto mbalimbali, ikiwemo ugumu wa kufundisha mlemavu kama huyu. MWISHO.

MBUNGE WA SINGIDA MASHARIKI TUNDU LISSU AKIWA AMEFUATANA NA MBUNGE WA ARUSHA MJINI GODBLESS LEMA AFANYA MKUTANO IKUNGI NA KUVALISHWA MGOLOLE NA KUPEWA MKUKI IKIWA NI ISHARA YA MTU SHUJAA.

WANANCHI wa Ikungi, Jimbo la Singida Mashariki wakimsikiliza Mbunge wa Jimbo hilo Tundu Lissu alipozungumza na Wananchi hao kwenye mkutano wa hadhara kuzungumzia mambo mbalimbali ikiwemo kuwashaishi vijana na wanawake kujiandika kwenye daftari la kudumu la kupigia kura.
TUNDU Lissu akiwa juu nya jukwaa kuwahutubia wananchi waliojitokeza kusikiliza hotuba yake aliyoitoa makao makuu ya wilaya Ikungi.
. AKILAKIWA na wananchi baada ya kuvikwa vazi la mgolole na kupewa ngao na mkuki ikiwa ni ishara ya mtu shujaa.
Singida Mei 12, 2014. MBUNGE wa Singida Mashariki Tundu Lissu amehimiza vijana, wanawake na walemavu kuzikabili changamoto zilizopo jimboni mwake kwa kujiandikisha kwa wingi kwenye daftari la kudumu la kupigia kura na kuwania nafasi balimbali za uongozi, ili watatue kero hizo wakiwa madarakani. Akizungumza na wananchi wa Ikungi Mjini, Mbunge huyo aliyeingia madarakani kupitia uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 kwa tiketi ya CHADEMA, Lissu alisema kuwa sasa umefika wakati kwa makundi hayo kuwania uongozi, badala ya kuwaachia watu wachache kujirudia kila chaguzi. “Ndugu zangu, hasa vijana na wanawake muda ukifika wa kujiandikisha hakikisheni mnatumia vizuri nafasi hii…tusione aibu kugombea nafasi hizi, tukishinda vizuri nafasi ya vitongoji, vijiji na mitaa itaturahisishia pia kushinda uchaguzi mkuu wa madiwani, wabunge na Rais hapo mwakani,”alisema Lissu. Aidha Lissu aliyechaguliwa mwishoni mwa wiki iliyopita na kiongozi wa kambi ya upinzani Freeman Mbowe kuwa waziri kivuli, wizara ya katiba na sheria (muungano), alisema wajumbe wa bunge la katiba kutoka upinzani hawatarudi kujadili muswada wa katiba, hadi hapo lugha chafu za matusi zitakapokoma bungeni. Mapema kwenye mkutano huo mbunge wa Arusha mjini Godbless Lema aliyefuatana na Lissu, aliwaeleza wananchi waliokusanyika makao makuu ya Wilaya ya Ikungi kuendelea kumpa ushirikiano mbunge wa jimbo hilo, ili aendelee kuwapigania. “Mbunge wenu ni mbunge wa taifa, mpeni nafasi afanye kazi ya kuwakomboa watanzania…akienda sehemu mbalimbali za nchi akasimama na kuzungumza, wananchi watamsikiliza na kumuelewa kwa sababu ni mtu wa watu, mpeni nafasi afanye kazi ya kuwatetea wananchi,”alisema. Katika ziara hiyo, Lissu alipokewa na wananchi wa jimbo lake katika kijiji cha Ulyampiti wilaya Ikungi akitokea bungeni Dodoma, na kuvishwa mgolole na akina mama kisha wazee wanaume wakamkabidhi ngao na mkuki, ikiwa ni ishara ya mtu shujaa. MWISHO.

Wednesday 7 May 2014

HALMASHAURI YA WILAYA MKALAMA YAPITISHA TASIMU YA SHERIA NDOGO KWA AJILI YA ADA NA USHURU KUONGEZA UFANISI WA UTEKELEZAJI WA KAZI ZAKE.

MWENYEKITI wa halmashauri Wilaya Mkalama Mkoani Singida James Mkwega akisisitiza jambo wakati wa maamuzi juu ya kupitisha rasimu ya sheria ndogo mbalimbali,ikiwemo ushuru wa kuku, samaki na mazao, wakati wa baraza la madiwani lililokutana makao makuu ya Wilaya hiyo, Nduguti.
Mwanasheria wa halmashauri ya Wilaya Mkalama Neto Mwambalasu akiwasilisha rasimu ya sheria ndogo ya ada na ushuru mbalimbali mbele ya baraza la madiwani kwenye kikao cha baraza hilo lililokutana makao makuu ya wilaya hiyo, Nduguti.
Baadhi ya madiwani wa halmashauri ya Wilaya Mkalama wakipitia makablasha yenye taarifa mbalimbali ikiwemo rasimu ya sheria ndogo kwa ajili ya ada na ushuru wa kuku, mazao na samaki ili kuiongezea halmashauri hiyo uwezo wa kutekeleza majukumu yake.
Singida Mei 07, 2014. ILI kuiongezea uwezo halmashauri ya wilaya Mkalama Mkoani Singida itaanza kutoza ushuru wa kuku,samaki na mazao mbalimbali. Mwanasheria wa halmashauri hiyo Neto Mwambalasu aliwaeleza wajumbe wa mkutano wa baraza la madiwani lililokutana Nduguti kuwa, utekelezaji wa ushuru huo utaanza kutozwa baada ya kusainiwa na waziri mwenye dhamana, waziri mkuu Mizengo Pinda. Hata hivyo baadhi ya madiwani walionyesha wasiwasi kuhusiana na ushuru wa kuku, lakini mwansheria huyo aliwatoa mashaka kwa maelezo kuwa, sana sheria hiyo itawahusu wafanyabiashara wanaonunua na kusafirisha au kuvusha nje ya Wilaya hiyo. “Nawaomba sana waheshimiwa msipate wasiwasi kuhusiana na rasimu hii…mfano!, ushuru wa kuku wa Sh.500 kwa kuku, hautamhusu moja kwa moja mwananchi wa kawaida, badala yake utahusisha zaidi wafanyabishara wanaonunua na kusafirisha kuku wengi, kwa ajili ya biashara,”alifafanua. Mazao mengine yanayoingia kwenye rasimu na kiwango kikiwa katika mabano ni, samaki aina ya perege (Sh. 300), kambale (Sh. 50), kamongo (Sh.50), ng’ombe, nguruwe na punda (Sh. 2,000), wakati mbuzi na kondooo watalazimika kulipiwa ushuru wa Sh.1,000, kwa mmoja. Kwa mujibu wa Mwansheria huyo, baadhi ya ada na ushuru huo mwingine utakaohusisha maeneo 18, ni mazao ya chakula na biashara, vizimba sokoni, machinjio, ushuru wa madini, ada ya idhini ya ujenzi, mazao ya nyuki na ushuru wa kupaki/kuegesha magari. Katika hatua nyingine, baraza hilo lilipitisha mapendekezo ya kuyagawanya baadhi ya maeneo kwa kuyapandisha hadhi, ikiwemo vitongoji, vijiji, kata na tarafa, ili kutoa fursa kwa wananchi kunufaika na huduma bora baada ya kusogezwa karibu zaidi. Baadhi ya maeneo yaliyopendekezwa kuwa kata ni Mkalama, Nkalakala, Kidarafa, Tatazi, Lukomo, Tumuli, Lyelembo, Ikungu, Kinampundu, Nkungi, Dominiki na Endasiku, wakati tarafa zitakazoongezeka ni Mwanga, Gumanga na Mkalama (iliyobadilishwa kutoka Ibaga kuwa Mkalama). MWISHO.

Monday 5 May 2014

KLABU YA WAANDISHI WA HABARI MKOA WA SINGIDA-SINGPRESS IMEKABIDHI MSAADA WA KIBINADAMU KWA SHULE MAALUMU YA IKUNGI MCHANGANYIKO YENYE WALEMAVU WA AINA MBALIMBALI WAPATAO 104

MWALIMU mkuu wa shule ya msingi Ikungi Mchanganyiko iliyopo wilaya Ikungi Mkoani Singida, Bw. Olvary Kamilly (kulia) akipokea sehemu ya msaada kutoka kwa mwenyekiti wa klabu ya waandishi wa habari mkoa Singida ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya uhuru wa vyombo vya habari duniani, wakati klabu hiyo ilipoamua kuadhimisha kwa kusaidia shule hiyo yenye wanafunzi 1,200, kati yao 104 wenye ulemavu aina mbalimbali. Msaada huo umejumuisha vitu mbalimbali ikiwemo sukari, unga wa sembe, ngano, kalamu, madaftari, ndoo za maji, mafuta ya kula, biskuti, pipi, sabuni za kufulia, sahani, vikombe nk, katika makabidhiano yaliyofanyika shuleni hapo.
Elisante John, Singida Mei, 2014. WALEMAVU wamekuwa wakinyanyaswa, kubaguliwa hata kutengwa kutokana na mwonekano wao tu tangu kuzaliwa, lakini katika kukabiliana na tatizo hili serikali imekuwa ikiwapatia elimu kuanzia shule ya awali hadi elimu ya juu, lengo ni kuiwezesha jamii hiyo kupata fursa zaidi ya ajira ndani na nje ya nchi. Shule ya msingi Ikungi mchangayiko iliyopo Wilaya Ikungi Mkoani Singida ni kati ya shule hizo chache za bweni nchini inayotoa taaluma kwa walemavu mbalimbali, wakiwemo wasioona, albino na viungo. Mwalimu mkuu wa shule hiyo Olvary Kamilly anawaeleza wanahabari wa Mkoa Singida waliofika shuleni hapo kukabidhi msaada wa kibinadamu uliogharimu zaidi ya Sh.laki nane, kama sehemu ya maadhimisho ya siku ya uhuru wa vyombo vya habari duniani kuwa kitengo hicho kilianzishwa mwaka 1980. Kamilly anasema kuwa shule hiyo pia inajumuisha wanafunzi wasiyo walemavu, ambao jumla yao kwa pamoja wanafikia wanafunzi 1,200, wakiwemo wavulana 458 na wasichana 646, huku walemavu pekee idadi yao ni 104. Alisema kati ya wanafunzi hao, Jumanne Ramadhani ni mlemavu wa macho na Julius Charles mlemavu wa mikono (hana kabisa mikononi), lakini ameonyesha uhodari mkubwa wa kuandika kwa kutumia miguu yake, huku Jumanne akisoma kwa ufasaha kwa kupapasa maandishi. Kwa upande wake Mwenyekiti wa klabu ya waandishi wa habari mkoani Singida Seif Takaza alipongeza jitihada zinazofanywa na walimu na wanafunzi wa shule hiyo katika kuhakikisha jamii ya walemavu inaandaliwa kwa ajili ya kukabili maisha ya kujitegemea siku za usoni. Takaza alisema kuwa msaada huo kutoka kwa wanahabari wa mkoa wa Singida ni mwendelezo wa klabu hiyo kusaidia watu wa makundi mbalimbali maalumu yanayoodhani kuwa yametengwa na jamii. Naye Juma Issah ambaye ni mwanafunzi mlemavu wa ngozi, kwa niaba ya wenzake wote aliwashukuru wanahabari wa mkoa wa Singida kutokana na ukarimu waliouonyesha mpaka wakachukua uamuzi wa kushirikiana nao katika maadhimisho hayo. Msaada huo, unga wa sembe, ngano, sabuni, mchele, madaftari, kalamu, mafuta ya kula, pipi, biskuti, sahani, vikombe,ndoo nk, ikiwa ni mwendelezo wa wanahabari hao kusaidia makundi maalumu, kama walivyofanya hivyo mwaka juzi kwa kusaidia jamii ya Wahdzabe, inayoishi wilaya ya Mkalama. MWISHO.

Thursday 1 May 2014

RAIS MSTAAFU AWAMU YA TATU BENJAMEN MKAPA, KUPITIA MFUKO WAKE WA TAASISI YA BENJAMIN MKAPA HIV.AIDS AMEKABIDHI NYUMBA 30 ZA WATAALAMU WA AFYA VIJIJINI MKOANI SINGIDA ZILIZOGHARIMU SH. 1,945,187,143

RAIS wa awamu ya tatu Benjamen Mkapa (katikati) mkuu mkoa Singida Dk. Parseko Kone (kushoto) na mwakilishi wizara ya afya na ustawi wa jamii Dk. Catherine Joachim, akizindua nyumba ya watumishi wa afya vijijini, kati ya 30 zilizogharimu zaidi ya Sh. Bilioni 1.9 kupitia mfuko wa ‘Mkapa Foundation’ kwa wilaya za Mkalama, Iramba, Singida, Ikungi na Manyoni Mkoani Singida.
Mkuu Mkoa Singida Dk. Parseko Kone akikabidhi hati ya nyumba kwa mganga mkuu Wilaya Iramba Dk.Japhet Simeo, baada ya rais mstaafu Benjamen Mkapa kukabidhi nyumba 30 za kisasa kwa ajili ya watumishi wa afya vijijini, zilizojengwa na taasisi ya Mkapa foundation, kwa wilaya za Mkalama, Iramba, Manyoni, Ikungi na Singida, kwenye makabidhiano yaliyofanyika kijiji cha Senenemfuru katika halmashauri ya wilaya Singida.
Rais awamu ya tatu, Benjamen Mkapa akikabidhiwa kibuyu na akina mama wa kijiji cha Senenemfuru Singida vijijini, kikiwa na maana ya upendo, kwenye hafla ya kukabidhi nyumba, kati ya 30 zilizojengwa na Mkapa foundation kwa halmashauri tano za mkoa wa Singida.
Mwonekano wa nyumba iliyojengwa na taasisi ya Benjamen Mkapa katika kijiji cha Senenemfuru halmashauri ya wilaya Singida, kati ya 30 zilizojengwa katika wilaya tano mkoani Singida kwa ajili ya watumishi wa afya vijijini kwa gharama ya Sh.1,945,187,143.
Na Elisante John, Singida April 01, 2014. RAIS mstaafu awamu ya tatu Benjamen W. Mkapa kupitia taasisi yake ‘Benjamen William Mkapa HIV/AIDS’ (BMAF), amekabidhi nyumba 30 zilizojengwa kwenye zahanati 13 na vituo vya afya viwili kwa gharama ya zaidi ya Sh. Bilioni 1. 9, katika halmashauri tano za Wilaya Mkoani Singida. Akikabidhi sehemu ya nyumba hizo kwenye hafla iliyofanyika kijiji cha Senenemfuru Singida vijijini, mzee Mkapa alishukuru wafadhili waliowezesha kazi hiyo, ukiwemo mfuko wa dunia wa kupambana na Ukimwi, kifua kikuu na malaria (Global fund), kwa kuonyesha imani na serikali ya Tanzania. “Binafsi ninafarijika kufahamu kwamba wananchi wanaohudumiwa na zahanati 15 ambazo nyumba hizi zimejengwa, wataendelea kufaidika na huduma bora za afya kutoka vituo hivyo kwa sababu watoa huduma wameboreshewa mazingira ya kazi zao,”alisema rais mstaafu. Nyumba hizo zimejengwa katika zahanati ya Misughaa na Mangonyi (Ikungi), Mkenge, Mpambaa na Senenemfuru (Singida), Ulemo Uwanza na kituo cha afya Ndago (Iramba), Kinyambuli na Dominiki (Mkalama), pia kituo cha afya Itigi, Idodyandole, Heka, Mpola na Chibumagwa (Manyoni). Baada ya kukabidhi, mzee Mkapa alitumia fursa hiyo kuhimiza halmashauri za wilaya husika kutunza vyema nyumba hizo na kutumika kwa matumizi yaliyokusudiwa na alizitaka kutenga bajeti ya kutosha kwa ajili ya matengenezo ya mara kwa mara ili zidumu, kuendelea kuwa madhubuti na kuvutia zaidi. “Hata hivyo, ili kuweza kuwa na huduma ya afya bora zaidi na kamilifu ni lazima kuwepo na zahanati yenye dawa, vifaa vya kutolea huduma na vipimo na uwepo wa wataalamu wa kutosha kulingana na ikama…wekeni mkakati kuhakikisha hayo yote yanazingatiwa na kutekelezwa,”alisisitza Mkapa. Kwa upande wake mwakilishi wizara ya afya na ustawi wa jamii Dk. Catherine Joachim aliishukuru taasisi hiyo na akasema kupitia mradi huo kwa mwaka wa pili sasa utahusisha ujenzi wa nyumba 220 za watumishi wa afya kwa mikoa ya Arusha, Ruvuma, Manyara, Pwani na Singida. Aliishukuru taasisi ya Mkapa kutekeleza kazi zake kwa ushirikiano mkubwa na serikali, mashirika binafsi, wadu wa maendeleo na jamii kwa ujumla, ikiwa na lengo la kuimarisha huduma za Ukimwi, afya ya mama na mtoto na masuala mengine ya afya kwa wataalamu waliopo maeneo ya vijijini. Aidha, afisa mtendaji mkuu wa taasisi Benjamen Mkapa Dk. Ellen Mkondya-Senkoro alisema kuwa BMAF mkoani Singida imekuwa ikichangia shughuli mbalimbali ikiwemo kuimarisha huduma za Ukimwi, afya ya uzazi na masuala ya watumishi wa afya tangu mwaka 2006. Aliyataja mafanikio mengine mkoani hapa kuwa ni pamoja na kuajiri watumishi wa afya 28, kufadhili wanafunzi tisa wanaosoma vyuo mbalimbali vya afya, kujenga wodi ya wazazi katika vituo vya afya, kusaidia magari matatu ya kubebea wagonjwa na kutoa mafunzo juu ya usimamizi wa raslmali watu. MWISHO.

Tuesday 29 April 2014

BASI LA KAMPUNI YA SUMRY LAPARAMIA NA KUUA WATU 19 WAKIWEMO ASKARI POLISI WANNE WALIKOKUWA KAZINI.

PICHA ZA Miili ya askari polisi wanne wa mkoa wa Singida, Boniface Magubika, Novatus Tarimo, Michael Mwakihaba na Jumanne Mwakihaba, ikiwa kwenye masanduku kwa ajili ya ibada ya kuagwa na mamia ya wakazi wa mji wa Singida kwenye viwanja vya line Polisi, tayari kwa kusafirishwa jana jioni kwenda kuzikwa katika mikoa yao walikozaliwa ikiwemo Kilimanjaro, Pwani, Iringa na Mbeya.
Na Elisante John, Singida Aprili 29, 2014. WATU 19 wamekufa, wakiwemo askari polisi wanne na wengine nane wamejeruhiwa vibaya baada ya kugongwa na basi la lililokuwa linatokea Mkoani Kigoma, kwenye eneo la kijiji cha Utaho Kata ya Puma Wilayani Ikungi, barabara kuu ya Sindida- Dodoma kilomita 15 kutoka Singida Mjini. Ajali hiyo ilitokea juzi usiku saa 2.45 na kulihusisha basi namba T 799 BET Nissan mali ya Kampuni ya Sumry, likitokea Kigoma kwenda jijini Dar es Salaam, likiendeshwa na Paulo Njilo mkazi wa jijini Dar es Salaam. Kamanda wa polisi Mkoa Singida Geofrey Kamwela alisema siku ya tukio hilo wananchi wakiwa na askari polisi wa doria walikuwa wamekusanyika pembezoni mwa barabara kuupakia mwili ya mtu mmoja mwendesha baiskeli aliyegongwa na lori na kufariki dunia. Alisema kuwa wakiwa katika harakati za kuupakia mwili huo kwenye gari la polisi namba PT 1424 huku likiwa limeegeshwa pembeni mwa barabara, gafla basi hilo lilikuja kwa kasi na kuwagonga wananchi hao na 15 dunia papo hapo, huku wengine watatu wakifariki dunia wakati wakipelekwa hospitalini. Akielezea tukio hilo, Kamwela alisema dereva wa basi baada ya kukaribia eneo hilo aliliona gari la polisi likiwa limepaki pembeni kushoto mwa barabara, lakini katika kulikwepa ndipo alipoparamia kundi la watu waliokuwa pamoja na askari na kuwagonga huku wengine wakipotez amaisha. Aidha alisema dereva wa basi hilo baada ya ajali hiyo aliendelea na mwendo hadi aliposimama kilomita 25 katika makao makuu ya wilaya Ikungi na kutokomea kusikojulikana, lakini juhudi za kumtafuta zinaendelea. Aliwataja askari waliokufa kuwa ni F.849 D/CPL Boniface Magubika wa CID Wilaya ya Singida, F.6837 Pc Jumanne Mwakihaba wa FFU Singida, G.7993 Pc, Novatus Tarimo wa ofisi ya RCO na G.8948 Pc, Michael Mwakihaba wa FFU Singida. Wengine waliokufa aliwataja kuwa ni afisa mtendaji kijiji cha Utaho Ramadhan Mjengi, Mwenyekiti wa kijiji Utaho Paul Hamis, Mwenyekiti wa kitongoji cha Utaho Ernet Salanga, Said Rajab, Usirika Itambu, Chima Mughenyi, Salim Juma, Abeid Ramadhan, Mwinyi Hamis, na Issa Hussein wote wakazi wa kijiji cha Utaho. Kamanda Kamwela alisema miili ya marehemu wengine wanne bado haijatambuliwa na ndugu zao na imehifadhiwa kwenye chumba cha maiti hospitali ya mkoa wa singida. Alisema majeruhi wawili wamelazwa katika hospitali ya Mkoa Singida na wengine sita wapo hospitali ya misheni Malikia wa Ulimwengu iliyopo Puma. Aidha miili ya askari polisi wote inatarajiwa kusafirishwa kwenda katika mikoa wanakotoka wakati wowote mara taratibu za kipolisi zitakapokamilika, ikiwa ni baada ya kuwasiliana na ndugu zao wa Rombo-Kilimanjaro, Pwani, Mbalizi Mbeya na Iringa. Akielezea ajali hiyo Kamanda Kamwela alisema awali majira ya sa 1:30 usiku ilitokea ajali ya mtembea kwa miguu Gerad Zefania aliyegongwa na lori na kufa papo hapo. Mmoja wa majeruhi aliyelazwa hospitali ya mkoa Singida Musa Mohammed alisema kuwa wakiwa wanasubiri kuupakia mwili wa marehemu Gerald, lilitokea kwa kasi basi hilo na ghafla lilikwepa gari la polisi lililokuwa limesimama kuelekea basi linakotoka, kisha kuparamia kundi la watu na tangu hapo hakujielewa hadi alipozinduka asbuhi jana hospitalini. Alisema kuwa uchunguzi zaidi wa ajali hiyo unaendelea ili kujua chanzo halisi cha tukio pamoja na kumtafuta dereva wa basi la Sumry ili aweze kuhojiwa na kasha hatua za kisheria zeweze kuchukuliwa dhidi yake.

Tuesday 22 April 2014

WANANCHI WA VIJIJINI WATAKA WAJUMBE WA BUNGE LA KATIBA KUREJEA BUNGENI ILI WAENDELEE NA MCHAKATO WA KATIBA.

KAMANDA wa Umoja wa Vijana Jumuiya ya Chama Cha Mapinduzi(UVCCM) kata ya Gumanga Bw. Emmanuel Mkumbo akizawadia washindi mbalimbali wa soka baada ya mechi iliyozikutanisha timu ya Gumanga FC na Ikungu FC na Gumanga kkushinda 5-0 na kufanikiwa kujipatia jezi seti moja huku Ikungu ikijipatia mpira mmoja. Hiyo ilikuwa ni sehemu ya sherehe za kuapishwa kwake kuwa kamanda wa Jumuiya ya UVCCM Kata ya Gumanga.
KAMANDA wa Umoja wa Vijana Jumuiya ya Chama Cha Mapinduzi(UVCCM) kata ya Gumanga Bw. Emmanuel Mkumbo akiwa amebeba mkuki, pinde na mishale baada ya kuapishwa na mgeni rasmi katibu wa CCM Wilaya Mkalama Mkoani Singida Amosi Shimba kwenye uwanja wa mpira wa miguu wa shule ya sekondari Gumanga.
Na Elisante John, Mkalama Singida Aprili 22, 2014. BAADA ya wajumbe wa bunge la katiba kususia vikao vinavyoendelea mkoani Dodoma, wananchi wa maeneo ya vijijini katika wilaya ya Mkalama (Singida) wamewaomba wajumbe hao warejee haraka bungeni, ili waendelee kushiriki mchakato wa kupata katiba mpya. Wakiongea katika kijiji cha Gumanga juzi, wakati wa kumwapisha kamanda wa Umoja wa Vijana (UVCCM)Emmanuel Mkumbo wa kata ya Guamnga Wilaya Mkalama, baadhi ya wananchi hao John Peter, Grace Yindi na Fred Mabena wamewataka wajumbe hao kutanguliza mbele utaifa kwanza. Walisema kuwa badala ya kususia vikao vya bunge la katiba linaloendelea Mkoani Dodoma, sasa ni vyema wakarejea haraka bungeni, ili kuharakisha uundwaji wa katiba mpya ambayo itawakomboa Watanzania. "Kinachoendelea bungeni Dodoma siyo kitu kizuri, wao wanafanya mzaha na kuleta usimba na uyanga...waache mzaha, wafahamu kuwa sisi ndiyo tuliowatuma huko bungeni ili watutengenezee katiba ambayo itatufaa sisi Watanzania wote,"alisema John Peter wa Kijiji cha Maelu. Naye Grace Yindi mkazi wa Kijiji cha Kinankamba alisema kuwa uamuzi waliouchukua wa kutoka na kususia vikao vya bunge siyo njia sahihi ya kutatua kero na wala wasidhani kuwa jamii itawasikiliza kutokana na mgomo huo. Kutokana na hali hiyo Fred Mabena mkazi wa kijiji cha Guamanga aliwataka wajumbe hao wasione aibu kurejea bungeni badala yake wafanye haraka ili waendeleze mchakato wa kupata katiba mpya itakayokuwa na maslahi kwa Watanzania wote. Naye Mkumbo akizungumza baada ya kuapishwa kwake, aliwataka vijana kujiepusha na wanasiasa wenye lengo la kuchochea machafuko na hatimaye kusababisha vurugu hapa nchini. "Nchi hii ni yetu wote, nawaomba sana vijana wenzangu msikubali kuwasikiliza wala kutumiwa na watu wa aina hii wenye nia mbaya na nchi yetu...wao wanachotaka ni vurugu tu, achaneni nao na wala msiwasikilize," alisema Mkumbo. Hata hivyo mgeni rasmi kwenye hafla hiyo katibu wa CCM Wilaya ya Mkalama Amosi Shimba alimwomba kamanda huyo wa UVCCM kata ya Gumanga kuhakikisha anawatumikia vijana wote wa kata hiyo, bila kujali itikadi ya vyama vyao vya siasa. MWISHO.

Tuesday 15 April 2014

MRADI WA UMEME UNAOTUMIA NGUVU YA UPEPO KUGHARIMU ZAIDI YA DOLA ZA KIMAREKANI MILIONI 285 SINGIDA.

NAIBU waziri wa nishati na mdini Stephen Maselle (kushoto) akisaini kitabu cha wageni katika eneo la uwezekezaji nishati ya umeme unaotumia nguvu ya jua unaotarajiwa kujengwa kwenye eneo la Kisaki chini ya kampuni ya Wind East unaofadhiliwa na nchi ya United Kingdom (UK), kulia kwake ni waziri wa nishati na mabadiliko ya hali ya hewa wa UK Gregory Barker, balozi wa UK hapa nchini Dianna Melrose, mkuu wa Mkoa Singida Dk. Prseko Kone (wa mwisho kushoto).
Wakiwa eneo la mradi lenye mkondo wa upepo mkali kwa ajili ya kuzalisha umeme unaotumia nguvu ya upepo. Na Elisante John, Singida Aprili, 2014. SERIKALI ya Uingereza imeiomba Tanzania kuharakisha mchakato wa kuharakisha ujenzi wa kuzalisha umeme unaotumia nguvu ya upepo Mkoani Singida, ambao utahifadhi pia mazingira, ili kupunguza tatizo la nishati hiyo nchini. Waziri wa nchi, wizara ya nishati na mabadiliko ya hali ya hewa wa Uingereza Gregory Barker (Mbunge) amesema hayo, alipotembelea eneo la uwekezaji umeme wa upepo, katika eneo la Kisaki, Mjini Singida. Naye naibu waziri nishati na madini Stephen Masele amelikumbusha shirika la umeme nchini (TANESCO) kukamilisha haraka mazungumzo kati yao na mwekezaji wa mradi huo kampuni ya Wind East Africa inayotarajiwa kutumia dola za Kimarekani zaidi ya Milioni 285 hadi kukamilika. Aidha mhandisi wa mradi huo Baptiste Bargés alisema ingawa mchakato huo unasuasua kuanza, lakini utakapoanza utasaidia sana kuongeza uwezo wa TANESCO wakati utakapounganishwa kwenye gridi ya taifa, wakati Mkuu wa Mkoa wa Singida Dk Parseko Kone alieleza kufurahishwa na wananchi wa eneo la kisaki katika kuukubali mradi huo ambao utaongeza sana nishati hiyo nchini. Kwa mujibu wa naibu waziri Masele, jumla ya megawati 2,700 hadi 3,000 zinatarajiwa kuzalishwa hadi ifikapo mwaka 2015, wakati kwa sasa ni megawati 1,500 tu, ndizo zinazozalishwa nchini. MWISHO.

MKUTANO MKUU WA WADAU WA MASHAURIANO MANISPAA YA SINGIDA JUU YA MASTER PLAN YA MJI HUO KWA MIAKA 20 IJAYO.

MADIWANI wa Manispaa ya Singida wakiwa kwenye picha ya pamoja na mkuu wa Mkoa wa Singida Dk. Parseko Kone (wa tatu kutoka kushoto mbele waliokaa), baada ya kufungua mkutano mkuu wa Master plan ya mji wa Singida kwa miaka 20 ijayo uliofanyika ukumbi wa chuo cha VETA Mjini Singida.
WENYEVITI wa mitaa Manispaa ya Singida wakiwa na mgeni rasmi Dk. Parseko Kone kwenye picha ya pamoja katika mkutano huo.
Hawa nao ni watendaji wa kata Manispaa ya Singida katika mkutano huo.
Meya wa Manispaa ya Singida Shekhe Salum MOhammed Mahami akishukuru baada ya ufunguzi wa mkutano huo uliofanywa na mkuu wa Mkoa wa Singida Dk. Parseko Kone.
Mkuu wa Mkoa wa Singida Dk. Kone akifungua mkutano huo.
Maofisa kitendo cha mipango miji Manispaa Singida wakiwa kazini katika mkutano huo.
Mkurugenzi wa Manispaa Singida Joseph Mchina (mbele kulia) akiwa na wajumbe wengine wakisikiliza kwa makini mada iliyokuwa inatolewa kwenye mkutano huo.